IQNA

Kufuatia Hukumu ya Mahakama

Ardhi ya Msikiti wa Babri nchini India yaporwa rasmi, yakabidhiwa Mabaniani

22:44 - November 09, 2019
Habari ID: 3472207
TEHRAN (IQNA) Mahakama Kuu ya India imewapokonya Waislamu ardhi ya Msikiti wa kihistoria wa Babri na kuwakabidhi Mabiniani (Wahindi) eneo hilo ili wajenge hekalu lao.

Mahakama hiyo imetoa hukumu hiyo ya kidhalimu na iliyojaa chuki leo  katika mazingira ya usalama mkali  huku vikosi vya usalama vikiwa vimewekwa katika hali ya tahadhari kote India.

Jopo la majaji watano waliopitisha uamuzi huo kwa kauli moja wakiongozwa na Jaji Mkuu Ranjan Gogoi, limeamua kuwapatia Mabaniani  eneo la ardhi hiyo iliyopo kwenye mji wa Ayodhya katika jimbo la Uttar Pradesh kaskazini mwa India, ambapo awali ulikuwepo msikiti wa kihistoria wa Babri kabla ya kubomolewa mwaka 1992 na Wahindu wenye misimamo ya kufurutu mpaka. Zaidi ya Waislamu 2,000 waliuawa katika machafuko yaliyosababishwa na kitendo hicho cha Wahindu kuubomoa msikiti huo.

Majaji hao wamedai kuwa msikiti huo uliokuwa umedumu kwa muda wa miaka 460, haukujengwa katika eneo tupu la ardhi, bali ulichukua nafasi ya hekalu lililokuwepo mahali hapo kabla yake.

Badala yake wamesema, Waislamu watapatiwa eneo jengine la ardhi yenye ukubwa wa eka tano kwa ajili ya kujenga msikiti mwingine.

Wakitoa maoni yao kuhusu hukumu hiyo iliyotangazwa leo na Mahakama ya Juu Kabisa ya India, Waislamu wa kada mbali mbali nchini humo wameeleza kutoridhishwa kwao na uamuzi huo na kueleza kwamba wataamua nini cha kufanya baada ya kuipitia hati kamili ya uamuzi wa mahakama.

Muhammad Musa, Muislamu mwenye umri wa miaka 58 wa eneo la Zakir Nagar amesema, mahakama haikutenda haki, lakini akaongezea kwa kusema:

"Inatupasa tuikubali hukumu yoyote iliyotolewa, kwa sababu tunaishi katika India inayoendeshwa na chama cha mrengo wa kulia cha BJP, ambacho kinadhani nchi hii ni milki ya Wahindu peke yao. Waislamu wanapaswa kuwa watulivu na kutochukua hatua yoyote, kwa sababu kuna nguvu zinazotaka utokee umwagaji damu nchini," ameeleza Musa.

Waziri Mkuu wa India Narendra Modi na maafisa wengine wa chama chake tawala cha BJP, wamepongeza uamuzi huo uliotolewa na mahakama ya juu kabisa ya nchi hiyo. Chama tawala cha BJP cha Mabaniani wenye misimamo ya kufurutu ada kimekuwa kikitekeleza sera za kuwakadamiza Waislamu India.

3469833

captcha