IQNA

Qur'ani Tukufu Inasemaje /15

Kaaba Tukufu, jumba la kwanza la Ibada katika historia

21:04 - July 02, 2022
Habari ID: 3475453
TEHRAN (IQNA) – Kaaba tukufu iliyoko Makka ni mahali ambapo Waislamu hutekeleza Hija na Umrah, lakini kwa mujibu wa Qur'ani, Kaaba ni kwa ajili ya mwongozo sio tu kwa Waislamu bali ulimwengu mzima.

Mwezi wa Dhul Hijja ni wakati wa ibada adhimu ya Hija. Ibada hii, Qur'ani Tukufu inasema, ilifanyika kwa mara ya kwanza wakati wa Nabii Ibrahim (Amani Iwe Juu Yake) na baada ya hapo Nabii huyu wa Mwenyezi Mungu alijenga Kaaba.

"Na pale tulipomweka Ibrahim pahala penye ile Nyumba tukamwambia: Usinishirikishe na chochote; na isafishe Nyumba yangu kwa ajili ya wanao izunguka kwa kut'ufu, na wanao kaa hapo kwa ibada, na wanao rukuu, na wanao sujudu. Na watangazie watu Hija; watakujia kwa miguu na juu ya kila ngamia aliye konda, wakija kutoka katika kila njia ya mbali.” (Surah Al-Hajj, aya za 26- 27)

Kinachovutia kuhusu Kaaba Tukufu  ni kwamba Mwenyezi Mungu (katika aya iliyotangulia) anaielezea kama ishara ya kwanza na Kibla cha kumwabudu Yeye na kisha anasisitiza umuhimu wa kuhiji. Pia kuna aya nyingine mbalimbali katika Qur'ani Tukufu kuhusu kanuni na maelezo ya ibada za Hijja.

Qur'ani Tukufu inasema katika aya ya 96 ya Surah Al Imran: "Hakika Nyumba ya kwanza walio wekewa watu kwa ibada ni ile iliyoko Bakka (jina jingine la Makka), iliyo barikiwa na yenye uwongofu kwa walimwengu wote."

Allamah Tabatabai mfasiri maarufu wa Qur'ani Tukufu anasema katika tafsiri yake ya  Al-Mizan ya Qur'ani Tukufu kwamba Al-Kaaba ni ya daraja zote za mwongozo na inaweza kusemwa kwamba hakuna yeyote anayweza kufika daraja hiyo isipokuwa mja wa Mwenyezi Mungu aliyetakasika. Mbali na wokovu wa Akhera, Kaaba inaongoza ulimwengu wa Kiislamu kwenye furaha ya dunia, ambayo ni umoja katika Umma wa Kiislamu.

Kaaba pia inawaongoza wasiokuwa Waislamu kwa kuwaamsha kwenye ukweli kwamba Uislamu umewaunganisha watu wa rangi na kaumu tofauti na kuunda udugu baina yao.

Kwa hivyo, umoja ni moja ya malengo ya kimsingi yanayofuatiliwa katika Hija

Kwa hiyo kuna mambo mawili hapa: Kwanza; Kaaba ni chanzo cha uongofu unaopelekea furaha katika dunia hii na ijayo, na pili; Kaaba ni mwongozo usio wa kundi fulani bali ni wa ulimwengu mzima.

Katika kufasiri aya ya 96 ya Surah Al Imran, Sheikh Muhsin Qara’ati katika Tafisiri ya Qur'ani ya Al Nur ameangazia nukta kadhaa, zikiwemo zifuatazo:

1 -  Al-Kaaba ndio mahali pa kwanza palipowekwa kwa watu kuabudu na kusali. (Nyumba ya kwanza (ya ibada) ambayo Mwenyezi Mungu aliwapa watu)

2-  Historia ya maeneo ya ibada ni miongoni mwa vigezo vya kubainisha thamani ya eneo hilo. (Nyumba ya kwanza ya ibada)

3-  Baraka za Kaaba sio tu kwa waumini au jamii maalum bali ni kwa watu wote. (Nyumba ya kwanza (ya ibada) ambayo Mwenyezi Mungu aliwapa watu (wote)

4-  Kuwa ni mahala pa watu wote ni ishara ya thamani kubwa ya  Kaaba. (... ambayo Mungu amewapa watu (wote))

5-  Kaaba ni chanzo cha uongofu kwa watu. (Ni yenye baraka na mwongozo kwa watu wote)

Habari zinazohusiana
captcha