Kwa mujibu wa mwandishi wa IQNA kutoka Dar es Salaam, mashindano hayo yamefanyika kwa himaya ya Idara ya Utamaduni ya Iran nchini Tanzania pamoja na Madrassatul Istiqama tarehe 23 Mei katika Masjid Hudaa eneo la Mbagala.
Katika mashindano hayo, wanafunzi wa kike na kiume kutoka madrassah tatu za Qur’ani za Al Manahil, Al Istiqama na Ar Ridhwan wameshindana katika kuhifadhi Qur’ani Tukufu kikamilifu.
Mashindano hayo yaliwashirikisha zaidi ya wanafunzi 100, maustadhi na waalimu wa Qur’ani kutoka maeneo kadhaa ya Dar es Salaam.
Akizungumza katika kikao hicho, mkuu wa Idara ya Utamaduni ya Iran nchini Tanzania Ali Baqeri amebainisha kuhusu fadhila na faida za kuhifadhi na kuisoma Qur’ani Tukufu na kusema Qur’ani Tukufu ni mhimili wa umoja wa Kiislamu. Aidha ameashiria kuhusu ustawi wa harakati za Qur’ani nchini Iran.Huku akiashiria kufanyika mashindano ya kimataifa ya Qur’ani Tukufu nchini Iran, amesema katika Mwez Mtukufu wa Ramadhani mwaka huu kutafanyika mashindano ya Qur’ani katika maeneo mbali mbali ya Tanzania na washindi watashiriki katika mashindano ya kimataifa ya Qur’ani nchini Iran mwakani.../mh