Baraza la mawaziri la utawala bandia wa Israel limekubaliana na mpango wa kusitisha vita na tayari usitishaji vita huo ulianza kutekelezwa usiku wa manane kuamkia Ijumaa ya leo kwa majira ya Ghaza.
Taarifa ya awali ilieleza kuwa, utawala haramu wa Kizayuni wa Israeli umeukubali mpango wa Misri wa kusitisha mapigano mabaya zaidi kuwahi kutokea tangu mwaka 2014, na imekubali bila masharti yoyote.
Taarifa zaidi zinasema kuwa, Misri sasa inatarajiwa kutuma wajumbe huko katika ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu na Ukanda wa Ghaza katika siku chache zijazo kwa lengo la kuumaliza kabisa mgogoro huu.
Tangu siku ya Jumatatu ya tarehe 10 Mei, jeshi la utawala ghasibu wa Kizayuni wa Israel limeanzisha mashambulio ya kinyama dhidi ya Wapalestina wa eneo la Ukanda wa Ghaza, ambapo hadi sasa Wapalestina wasiopungua 230, wakiwemo watoto 65 wameshauawa shahidi kutokana na mashambulio hayo na wengine zaidi ya 1,500 wamejeruhiwa.
Katika kujibu uchokozi na jinai hizo za kinyama za utawala haramu wa Israel dhidi ya Ghaza, makundi ya muqawama ya Palestina yamevurumisha maelfu ya makombora kuelekea miji na vitongoji haramu vya utawala ghasibu wa Kizayuni katika ardhi za Palestina unayoikalia kwa mabavu na kuusaabbishia hasara kubwa ambayo haijawahi kupata katika historia ya vita na Waarabu.