Sayyid Ebrahim Raisi, Rais mpya wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ameyasema hayo leo Ijumaa hapa Tehran katika mazungumzo yake na Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Yustino Ndugai na mwenzake wa Zanzibar, Zubeir Ali Maulid.
Raisi ameashiria uhusiano wa kifariki na kidugu baina ya pande mbili hizo na kusisitiza kuwa: Kwa kuzingatia fursa nzuri na pia ukuruba wa kihistoria baina ya mataifa haya mawili, hususan Washirazi wa Zanzibar, lazima tuimarishe kiwango cha uhusiano na ushirikiano wetu.
Rais Raisi amesema anatumai kuwa, uhusiano wa kibunge baina ya Majlisi ya Ushauri ya Kiislamu (Bunge la Iran) na mabunge ya Tanzania na Zanzibar utasaidia kustawisha ushirikiano wa pande mbili na maingiliano ya kieneo baina ya nchi mbili.
Katika mkutano huo, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Yustino Ndugai na mwenzake wa Zanzibar, Zubeir Ali Maulid sanjari na kuwasilisha salamu za pongezi kwa Rais mpya wa Iran kutoka kwa marais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Zanzibar, wamesema wanatumai ukurasa mpya wa uhusiano wa Dar es Salaam na Tehran utafunguliwa.
Maspika hao wa Tanzania na Zanzibar wamegusia pia juu ya hamu ya Tanzania ya kuimarisha uhusiano na Iran katika nyuga tofauti hususan uga wa kiuchumi.
Kadhalika wameashiria kuhusu historia ya Washirazi wa Zanzibar wakati wa mapambano ya kujipatia uhuru Tanzania na kueleza kuwa, chama cha 'Afro-Shirazi' kilikuwa na mchango mkubwa wa kujikomboa katika nchi hiyo ya Afrika Mashariki.
Maspika hao wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Zanzibar ni miongoni mwa viongozi kutoka nchi mbalimbali duniani walioitembelea Tehran kwa ajili ya kuhudhuria hafla ya kuapishwa Rais wa nane wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.